LILE dili la bilioni 3 limeota mbawa. Ndicho unachoweza kusema baada ya miamba ya soka ya Libya Al Ettihad kuachana na mpango wa kumsajili straika wa Yanga, Clement Mzize na badala yake kunasa saini ya raia wa Botswana.
Nyota huyo amejiunga na kikosi hicho akitokea AS FAR Rabat ya Morocco aliyojiunga nayo Januari mwaka jana akitokea USM Alger ya Algeria, ambako tangu ajiunge na miamba hiyo amecheza jumla ya michezo 21 na kufunga mabao matatu tu msimu huu.
Timu nyingine alizowahi kuchezea nyota huyo ni Olympique Khouribga ya Morocco na Township Rollers na Gaborone United za kwao Botswana, huku akishinda taji la Kombe la Shirikisho Afrika msimu wa 2022-2023 na USM Alger, sawa na CAF Super Cup 2023.
Kitendo cha Tumisang Orebonye, kutua kwa miamba hiyo, kimefanya dili la Mzize kukwama, licha ya kiasi kikubwa cha fedha ambacho Yanga ingekipata, huku ikielezwa viongozi walikuwa tayari kumuuza, ingawa sio kipindi hiki wanachowania taji la Ligi.
Mzize amekuwa na kiwango bora akiwa na Yanga anayoitumikia kwa misimu mitatu sasa ambapo hadi sasa amefunga mabao tisa ya Ligi Kuu akiongoza mbio za ufungaji bora, huku akiasisti mengine matatu kati ya mabao 42 yaliyofungwa na timu hiyo katika mechi 17 za Ligi Kuu Bara.
Mbali na mabao hayo ya Ligi Kuu, Mzize pia amefunga mabao matano na asisti mbili katika Ligi ya Mabingwa Afrika ambapo Yanga ilitolewa hatua ya makundi na kukwama kutinga robo fainali kwa msimu wa pili mfululizo baada ya msimu uliopita kufika baada ya kupitia miaka 25 tangu ilicheza 1998.
Mzize ambaye ni zao la timu ya vijana ya Yanga, alikuwa akiwindwa na Al Ittihad iliyotenga ada ya uhamisho Sh3 bilioni, huku ada yake binafsi ya kusaini mkataba (sign-on fee), ikiwa ni zaidi ya Sh1.3 bilioni kwa mkataba wa miaka miwili.
Kuonyesha umuhimu na mchango wa nyota huyo, mbali na kiasi chote cha fedha alichokuwa amewekewa na Walibya, pia alitengewa kiasi cha mshahara wa Sh50 milioni kwa mwezi ambao kwa mkataba wake wa miaka miwili angevuna Sh1.2 bilioni, na ilipomkosa wakaamua kumnyakua Orebonye.