Ubalozi wa Tanzania nchini Marekani umethibitisha kuwa Watanzania 24 wanashikiliwa na Mamlaka ya Uhamiaji na Forodha ya Marekani (ICE) kwa kuishi nchini humo bila vibali halali.
Ubalozi umesema kati ya hao, wanne wamekamilisha taratibu zote za kisheria za kurejeshwa nchini na wanatarajia kurudishwa Tanzania wakati wowote na wengine 20 bado wanaendelea na kesi za uhamiaji nchini Marekani.
Ubalozi umeeleza kuwa haujapewa taarifa rasmi kuhusu tarehe maalum ya kurejeshwa kwa Watanzania hao, lakini tayari umeombwa kutoa hati za kusafiria kwa wawili kati ya wanne waliopangiwa kurejeshwa. Hii inaashiria kuwa mchakato wa kuwarejesha unaweza kufanyika wakati wowote.