
Habari kutoka chanzo ndani ya Azam FC zinafichua kwamba Ibenge ameamua kuachana na ofa ya Mali baada ya Azam kumuongezea thamani ya mkataba wake yakiwemo malipo.
Mbali na mshahara huo pia kocha huyo ameboreshewa vipengele vingi vya bonasi zake endapo ataiwezesha kubeba mataji au kufika hatua ya juu zaidi kwenye mashindano ya Afrika msimu ujao.
“Ibenge ni kocha mkubwa na Azam imempa heshima kubwa. Walimuita na kumkumbusha namna wanamuhitaji kwa ajili ya mradi waliouanza msimu huu na kwamba klabu bado inamuhitaji ndio maana ilimuita mezani mapema ikazungumza juu ya mkataba mpya.
“Yeye amefurahi kubaki hapa kutokana na utulivu wa mazingira ya kazi ambayo ameyapata hapa tangu amefika,” kimefichua chanzo ndani ya klabu hiyo.
Aidha chanzo hicho kimeeleza kuwa Ibenge amevutiwa na namna alivyohakikishiwa nafasi kubwa ya kufanya maamuzi ya kila kitu kuhusu kikosi chake likiwemo suala la usajili wa wachezaji.
“Lingine ni uongozi kuamua kwamba maamuzi yoyote kuhusu mambo ya ufundi yataanzia kwake kila kitu kitatokana na mapendekezo yake. Na hili hatalisubiri kuliona kwenye mkataba wake mpya lakini ameshaliishi hapa ndani ya mwaka wake huu wa kwanza,” kimefichua.
Aidha Ibenge amekubaliana na mahitaji ya Azam inayotaka kufika mbali kimataifa kwa msimu ujao, ambapo kocha huyo mkongomani ameridhika na kila kitu akisema anataka kuendelea kuwa sehemu ya mabadiliko ya klabu hiyo.
“Unajua kwa mara ya kwanza tumecheza hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho msimu huu tukiwa na Ibenge. Na kuna mambo klabu itayahitaji likiwemo kufika mbali zaidi kimataifa na kocha amekubaliana na hilo kuwa linawezekana,” kimesema chanzo hicho.
Mtendaji Mkuu Msaidizi wa Azam FC, Rashid Seif amesema kuwa suala la Ibenge kuongezewa mkataba lilikuwa rahisi kwa sababu lilishakuwa katika makubaliano yao.
“Alipokuja alipewa mkataba wa mwaka mmoja ambao ulikuwa na kipengele cha kuongeza miwaka miwili pindi utakapomalizika. Mengine yote kuhusu maslahi na mengineyo yalishakuwa katika hayo makubaliano.
“Klabu inaona mueleke wa timu chini ya Ibenge ni sahihi na ndio maana tumeamua kuendelea naye,” amesema Seif.
