Aliyedai fidia ya Sh40 milioni kwa kulea mimba ya mtoto asiye wake, agonga mwamba kortini

 

Aliyedai fidia ya Sh40 milioni kwa kulea mimba ya mtoto asiye wake, agonga mwamba kortini
Aliyedai fidia ya Sh40 milioni kwa kulea mimba ya mtoto asiye wake, agonga mwamba kortini

 

Aliyedai fidia ya Sh40 milioni kwa kulea mimba ya mtoto asiye wake, agonga mwamba kortini

Omary alidai Sh10 milioni alizotumia katika huduma za ujauzito na kujifungua, pamoja na Sh30 milioni alizodai kutumia kumlea na kumsomesha mtoto huyo hadi kufikia utu uzima.

Alidai aligundua mwaka 2021, kwamba mtoto huyo ambaye wakati huo alikuwa na miaka 24, hakuwa wake. Pia, aliiomba mahakama iamuru kuondolewa kwa ubini wake katika nyaraka za mtoto huyo.

Hata hivyo, Mahakama Kuu, Masjala Ndogo ya Singida imetupilia mbali rufaa yake na kusimamia uamuzi wa Mahakama ya Wilaya ya Singida uliokataa madai hayo.

Katika hukumu iliyotolewa Agosti 14, 2026 na Jaji, Ayoub Mwenda na kuwekwa kwenye tovuti ya Mahakama Agosti 17, 2026, ilieleza Omary alishindwa kuthibitisha kuwa alifichwa ujauzito huo.

Jaji alisema madai ya kurejeshewa fedha yangekuwa na msingi kama Hadija angeuficha ujauzito wakati wa ndoa, lakini ushahidi ulionyesha Omary alikuwa akijua hali hiyo.

“Nimepitia ushahidi uliopo na sijaona kasoro katika hitimisho la mahakama ya chini. Kama ilivyoelezwa kwa usahihi na mahakama ya chini, mdaiwa angeweza kuhukumiwa kwa kosa la kuficha ujauzito iwapo tu, katika siku ya harusi angeulizwa kama ana ujauzito au la, jambo ambalo halikutokea,” alisema.

Kwa mujibu wa Jaji Mwenda, kumbukumbu za kesi zinaonyesha swali aliloulizwa Hadija siku ya ndoa lilikuwa kama alikuwa tayari kufunga ndoa na Omary.

“Hakuna sheria inayomlazimisha mwanamke kusema kwa hiari kama ana mimba wakati wa kujiandaa kufunga ndoa ikiwa hajaulizwa,” alisema.

Hivyo, Jaji alisema ushahidi ulionyesha Hadija alimweleza Omary kabla ya ndoa kwamba alikuwa na ujauzito wa mwanaume mwingine.

Hadija katika utetezi wake alisema wakati Omary alipokuwa akimchumbia, alimweleza kuwa alikuwa na mwanaume mwingine aliyempa ujauzito, lakini Omary alisisitiza kumuoa akisema nyumba ya ndoa haizai mtoto haramu.

Walipofunga ndoa mwaka 1997, Hadija alikuwa na ujauzito wa miezi minne hadi mitano na alijifungua Oktoba 10, 1997.

Awali alimpa mtoto jina Mohamed Joseph, lakini Hadija alieleza kuwa Omary ndiye aliyesisitiza jina libadilishwe na baadaye mtoto akaitwa Juma Omary Juma Mgana.

Katika madai yake, Omary alisema alimtunza mtoto huyo akiamini ni wake, akigharamia huduma za ujauzito, kujifungua, malezi na elimu.

Alisema mwaka 2021 ndipo Hadija alipomweleza kuwa mtoto huyo si wake. Hata hivyo, katika shauri la talaka namba 14 la 2024, mahakama ilimwamuru kuendelea kumhudumia mtoto huyo kwa kutumia mapato ya kodi ya nyumba kugharamia matibabu na elimu hadi atakapofikia utu uzima.

Omary pia alidai kuwa mwaka 2006 Hadija alibadili msimamo na kutangaza kuwa Juma hakuwa mtoto wake, jambo lililosababisha mtoto huyo kuhamishiwa kwa mjomba wake na baadaye shangazi yake.

Juma aliyetoa ushahidi kama shahidi wa pili wa utetezi, alikanusha kupokea fedha kutoka kwa Omary kwa ajili ya elimu, akisema alisoma shule ya Serikali ambayo haikuwa na ada.

Jaji Mwenda pia alikataa madai ya Omary kwamba alitumia Sh1.5 milioni kumlipia Hadija gharama za kujifungua, akisema hakuwasilisha ushahidi kuthibitisha fedha hizo zilitumika kwa matibabu.

Kuhusu madai ya matumizi ya fedha za kodi, Jaji alisema katika shauri la talaka mahakama iligawa nyumba kwa asilimia 50 kwa 50, hivyo mapato yake hayakuwa ya mtoto huyo pekee.

“Hata kama mdaiwa asingekuwa na sehemu ya asilimia 50 ya nyumba hiyo, jambo ambalo si kweli, mlalamikaji alishindwa kuwasilisha ushahidi wowote kuthibitisha mdaiwa alikuwa akikusanya kiasi cha Sh225,000 kwa mwezi kama ilivyodaiwa,” alisema.

Jaji pia alisema Omary hakuthibitisha hasara au madhara halisi yaliyosababishwa na mwenendo wa Hadija.

“Msongo wa mawazo pekee, bila uthibitisho, hauwezi kuwa sababu halali ya kutoa fidia ya jumla,” alisema.

Aliongeza kuwa kwa kuwa Omary alijua ujauzito huo kabla ya ndoa, hakukuwa na udanganyifu uliosababisha hasara au madhara.

“Kama ilivyobainishwa kwa usahihi na mahakama, mtoto huyo alilelewa kama sehemu ya familia; hivyo, madai ya kurejeshewa gharama hayana msingi wa kisheria. Rufaa hii inakataliwa na uamuzi wa Mahakama ya Wilaya unasimama,” alisema.

Hata hivyo, kuhusu gharama za kesi, Jaji alisema kwa kuwa pande hizo bado zinashirikiana katika kulea watoto wengine, haikuwa mwafaka kumuamuru Omary kuzilipa kwa kuwa hatua hiyo isingeleta amani na maelewano katika familia ambayo imesambaratika.

Related Posts