Uwanja wa Yanga Mambo Safi, Hersi Said Afunguka Ramani Yote

Rais wa Klabu ya Yanga SC, Eng. Hersi Said, amefunguka kwa kina kuhusu dira ya klabu hiyo katika kipindi hiki cha mageuzi makubwa, akieleza kwa msisitizo dhamira ya kujenga uwanja wa kisasa utakaokuwa nyumbani rasmi ya mabingwa hao wa kihistoria. Katika maelezo yake, alibainisha kuwa Yanga haijajikita tu katika mafanikio ya uwanjani, bali pia katika kuweka misingi imara ya muda mrefu itakayoifanya klabu hiyo kuwa taasisi thabiti na ya mfano barani Afrika.

Akizungumzia azma ya ujenzi wa uwanja mpya, Eng. Hersi alisema, “Tunapotazama mbele Yanga SC matarajio yetu yapo wazi, tumejitolea kujenga uwanja wa kisasa wa nyumbani Jangwani unaoakisi historia yetu.” Kauli hiyo inaonesha dhamira ya dhati ya uongozi wa klabu kuhakikisha Yanga inakuwa na miundombinu ya kisasa itakayokidhi mahitaji ya ushindani wa kimataifa na kuwapa mashabiki wao mazingira bora ya kushuhudia timu yao.

Mbali na suala la uwanja, Rais huyo aligusia pia malengo mapana ya klabu katika anga la kimataifa. Alisisitiza kuwa Yanga imelenga kupiga hatua zaidi barani Afrika na kuitangaza vyema Tanzania kupitia mafanikio ya michezo. “Yanga tumejidhatiria kupata mafanikio makubwa zaidi barani na kuinua taswira ya soka la Tanzania Duniani kote,” alisema kwa kujiamini. Kauli hiyo inaakisi dhamira ya kuifanya Yanga kuwa balozi wa soka la Tanzania katika majukwaa ya kimataifa.

Eng. Hersi pia alieleza kuwa mafanikio hayo hayawezi kupatikana bila kuweka mifumo bora ya kiutawala na kifedha. Alifafanua kuwa katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, klabu imefanya maboresho makubwa ya ndani. “Katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita, Yanga SC tuliboresha mifumo ya utawala ili kuendana na viwango vya kitaaluma na kuhakikisha uwajibikaji, pia tulimarisha msingi wetu wa kibiashara ili kujenga uimara wa kifedha.” Hii inaonesha kuwa mabadiliko yanayoendelea ndani ya klabu hayalengi matokeo ya muda mfupi pekee, bali uendelevu wa muda mrefu.

Katika hatua nyingine ya mageuzi, uongozi wa Yanga ulifanya mabadiliko ya nembo na kuanzisha Shule ya Soka ya Yanga kama sehemu ya mkakati wa kuwekeza kwa vijana. “Zaidi ya hayo, tulibuni chapa ya Yanga SC na kukubali mabadiliko ili kuileta klabu karibu na mashabiki wake kote Tanzania na duniani kote, lakini pia tulizindua Shule za soka za Yanga kama uwekezaji wa kimkakati katika maendeleo ya vijana, kuhakikisha kwamba mustakabali wa klabu unajengwa kutoka ndani na chini,” aliongeza. Hii inaonesha kuwa klabu inalenga kujenga kizazi kipya cha wachezaji kitakachodumisha ubora wake kwa miaka mingi ijayo.

Kuhusu mafanikio ya kimashindano, Eng. Hersi alikumbusha kuwa Yanga imefuzu hatua ya makundi ya CAF Champions League mara tatu mfululizo, jambo alilolitaja kama mafanikio ya kihistoria. “Kwa upande wa mwingine tumefuzu hatua ya makundi ya CAF Champions League mara tatu mfululizo mafanikio ya kihistoria kwa soka la Tanzania na ishara tosha ya ushindani wetu katika bara la Afrika.”

Related Posts