
Uchambuzi mpya wa kiuchumi umeonesha kuwa shilingi ya Tanzania imeendelea kuwa imara licha ya kuongezeka kwa deni la taifa, hali inayotajwa kuchangiwa na uwepo wa akiba ya fedha za kigeni, mikakati madhubuti ya sera za fedha unaofanywa na Benki Kuu ya Tanzania pamoja na udhibiti wa mikopo ya ndani.
Kwa mujibu wa uchambuzi huo uliofanywa na Taasisi ya Utafiti wa Kiuchumi ya TICGL wa mwezi Desemba 2025, thamani ya Shilingi ya Tanzania imeonesha utulivu mkubwa dhidi ya Dola ya Marekani, ambapo wastani wa ubadilishaji ulifikia Shilingi 2,452.76 kwa dola moja, huku kiwango cha kushuka kwa thamani ya fedha hiyo kwa mwaka kikiwa asilimia 1.3 pekee, kiwango kinachotajwa kuwa kidogo ukilinganisha na nchi nyingine za ukanda huo.
Taarifa hiyo inaeleza kuwa deni la taifa limefikia shilingi trilioni 134.9, ambapo sehemu kubwa ya deni hilo ni la nje linalochukua takribani asilimia 69.5 ya jumla ya madeni yote, huku deni la ndani likichangia asilimia 30.5.
