Mfanyabiashara Rostam Ainunua Nation Media ya Kenya


Baada ya zaidi ya miaka 66 ya ushirikiano wa kihistoria katika tasnia ya habari Afrika Mashariki, hatua mpya imeanza kufuatia uamuzi wa Aga Khan Fund for Economic Development (AKFED) kuuza hisa zake katika kampuni ya NPRT Holdings Africa Limited.

‎AKFED imetangaza kuuza hisa zake zote katika NPRT Holdings Africa Limited, inayomiliki asilimia 54.08 ya hisa za Nation Media Group (NMG), kwa kampuni ya Taarifa Ltd inayomilikiwa na mfanyabiashara wa Afrika Mashariki, Rostam Azizi.

‎Hatua hiyo inahitimisha safari iliyoanza mwaka 1959 wakati vyombo vya habari vya Nation vilipoanzishwa kwa lengo la kujenga vyombo vya habari huru na vinavyoaminika Afrika Mashariki. Kilichoanza kama gazeti la Kiswahili *Taifa Leo* kimekua na kuwa kundi kubwa la vyombo vya habari lenye zaidi ya chapa 30 na kufikia zaidi ya watumiaji milioni 62 wa kidijitali katika nchi kadhaa za ukanda huu.

‎Katika historia yake, NMG imekuwa nguzo muhimu katika kuimarisha demokrasia na utoaji wa taarifa sahihi kwa jamii, kuanzia uzinduzi wa *Daily Nation* mwaka 1960, kuorodheshwa katika soko la hisa la Nairobi mwaka 1973, hadi kuongoza mageuzi ya habari za kidijitali barani Afrika.

‎Kupitia uwekezaji mpya wa Taarifa Ltd, NMG inatarajiwa kuimarisha zaidi mageuzi ya kidijitali, kuongeza ubunifu katika uandishi wa habari na kuendelea kuhudumia jamii kwa taarifa zenye maslahi ya umma.

‎Wakati huo huo, taasisi za mtandao wa Aga Khan zitaendelea kukuza taaluma ya uandishi wa habari kupitia Aga Khan University – Graduate School of Media and Communications, inayofundisha kizazi kipya cha wanahabari barani Afrika.

‎Mabadiliko hayo yanatarajiwa kukamilika ndani ya miezi mitatu hadi minne ijayo baada ya kupatikana kwa idhini zote za kisheria.

Related Posts