
Kesi mpya kuhusu kifo cha Gwiji wa soka wa Argentina, Diego Maradona, imeanza tena nchini Argentina, takribani mwaka mmoja baada ya kesi ya awali kuvunjika kufuatia kashfa iliyomuhusisha mmoja wa Majaji waliokuwa wakiisimamia.
Maradona, ambaye anachukuliwa kuwa mmoja wa Wachezaji bora zaidi kuwahi kutokea duniani, alifariki dunia Mwezi Novemba mwaka 2020 akiwa na umri wa miaka 60. Taarifa zinaeleza kuwa alikufa kutokana na Moyo kushindwa kufanya kazi sambamba na uvimbe wa mapafu.
Timu yake ya matibabu, inayoundwa na watu saba, inakabiliwa na Mashtaka ya kile ambacho waendesha mashtaka wamekitaja kuwa uzembe mkubwa katika utoaji wa huduma za afya kwa nyota huyo wa zamani wa soka.
Kesi ya kwanza ilisimama baada ya kuendelea kwa miezi miwili na nusu, huku mashahidi mbalimbali, wakiwemo watoto wa Maradona, wakitoa ushahidi wa kugusa hisia na kuibua hisia kali Mahakamani.
Mwezi Mei 2025, kesi hiyo iliahirishwa baada ya kubainika kuwa mmoja wa Majaji, Julieta Makintach, alihusika katika maandishi yanayohusiana na kesi hiyo, jambo lililodaiwa kukiuka maadili ya kazi ya kimahakama.
Baadaye, Jaji Makintach mwenyewe alishtakiwa kufuatia tuhuma hizo.
Katika kesi hii mpya, Mahakama inatarajiwa kusikiliza ushahidi kutoka kwa mashahidi 120, huku lengo kuu likiwa ni kubaini iwapo timu ya madaktari wa Maradona inawajibika kwa kifo chake.
