BMT Yathibitisha Kupitisha Katiba Mpya ya Simba, Yataka Itumike

BMT Yathibitisha Kupitisha Katiba Mpya ya Simba, Yataka Itumike
BMT Yathibitisha Kupitisha Katiba Mpya ya Simba, Yataka Itumike

BMT Yathibitisha Kupitisha Katiba Mpya ya Simba, Yataka Itumike

Baraza la Michezo la Taifa, BMT, limetoa ufafanuzi kwa umma, wanachama na wadau wa Klabu ya Simba kuhusu utekelezaji wa Katiba iliyorekebishwa ya klabu hiyo iliyoidhinishwa tarehe 18 Februari, 2026, hatua inayokuja baada ya mashabiki na wanachama wa klabu ya hiyo kulalamima kuhusu utekelezaji wa katiba mpya.

Taarifa iliyotolewa leo Agosti 19, 2026 na Katibu Mtendaji wa BMT, Neema Y. Msitha, imeeleza kuwa marekebisho ya Katiba ya Simba yalipitishwa na Mkutano Mkuu wa Wanachama wa Klabu ya Simba mnamo Novemba 30, 2025, na kuwasilishwa kwa Msajili wa Vyama na Vilabu vya Michezo kwa uchambuzi na kuidhinishwa kwa mujibu wa sheria na kanuni husika ambapo baada ya uchambuzi huo, BMT kupitia Msajili ilikabidhi rasmi Katiba hiyo kwa Simba ili ianze kutumika.

Taarifa hiyo imeeleza kuwa Serikali imefafanua kuwa ilikamilisha wajibu wake wa kuidhinisha na kukabidhi Katiba hiyo na kuanzia hapo, wajibu wa kutekeleza Katiba na kukamilisha mabadiliko yaliyopitishwa na wanachama ni wa Klabu ya Simba yenyewe na kusisitiza kuwa utekelezaji wa maamuzi yaliyomo katika Katiba hiyo haupaswi kufanywa na Serikali kwa niaba ya Klabu, kwa kuwa ni maamuzi yaliyofanywa na wanachama kupitia Mkutano Mkuu na kuidhinishwa kwa mujibu wa sheria.

Hata hivyo, Serikali inatambua kuwa utekelezaji wa mabadiliko hayo unaweza kuibua masuala ya utaratibu unaohitaji ufafanuzi. Kwa hiyo, BMT na taasisi nyingine husika za Serikali ziko tayari kuipokea Klabu ya Simba kwa ajili ya kutoa ufafanuzi wa utaratibu pale inapohitajika, kwa mujibu wa mamlaka ya kila taasisi.

Hivyo, Serikali inatoa wito kwa Klabu ya Simba kutumia vyombo na taratibu zake halali kukamilisha utekelezaji wa Katiba iliyoidhinishwa, na kuwasilisha rasmi kwa mamlaka husika masuala yoyote yanayohitaji ufafanuzi.

Serikali itaendelea kutekeleza jukumu lake la kuendeleza sekta ya michezo kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu, huku ikilenga maendeleo ya vilabu na sekta ya michezo kwa ujumla wake.

Ni matarajio ya Serikali kuwa masuala ya maendeleo ya michezo yataendelea kushughulikiwa kwa kuzingatia utulivu, uwazi, uwajibikaji maslahi ya wananchi na wapenzi wa michezo.

Related Posts