10 wakamatwa Morogoro tuhuma utapeli mtandaoni

10 wakamatwa Morogoro tuhuma utapeli mtandaoni
10 wakamatwa Morogoro tuhuma utapeli mtandaoni

JESHI la polisi mkoani Morogoro limewashikilia watu 10 kwa tuhuma za utapeli wa kutumia mitandao ya simu huku saba kati yao wakiwa na laini 110 zilizosajiliwa kwa majina ya watu tofauti katika maeneo ya Ifakara wilayani Kilombero.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi Morogoro (SACP) Alex Mkama watuhumiwa hao walikamatwa Machi 3, mwaka huu kwa nyakati tofauti baada ya oparesheni maalum iliyofanyika katika kitongoji cha Magoha Kata ya Lumemo wilayani humo.

Katika hatua nyingine, Nyamhanga Mwita (28) mkazi wa Ruaha wilayani Kilosa amekamatwa pia akiwa na kadi 148 za benki ambazo zina majina ya watu wa utambulisho tofauti ambazo anazitumia kuingia kwenye akaunti na kuchukua pesa isivyohalali.

Kamanda Mkama amesema uchunguzi wa awali umebaini kuwa waathirika wa matukio hayo ni wafanyabiashara wakubwa wa mazao ya chakula kutoka Mikoa ya Mwanza, Pwani, Dar es Salaam, Tanga, Zanzibar na Dodoma.

Kamanda huyo amesema upelelezi zaidi unaendelea ili kuwakamata washirika zaidi wa mtandao huo na kukomesha vitendo hivyo mkoani hapa.

Related Posts